MGODI WA SINGIDA GOLD MINE UMEZALISHA KG 49 ZA DHAHABU.

Singida

Imeelezwa kuwa, Mgodi mpya wa uchimbaji dhahabu wa Kati wa Singida Gold Mine unaomilikiwa na Kampuni ya Shanta Gold Mining Company Limited uliopo wilaya ya Ikungi mkoani Singida  umezalisha zaidi ya kilo 49 za dhahabu tangu kuanza uzalishaji mwezi Machi, 2023.

Akizungumza katika mgodi huo, Kaimu Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Singida Mjiolojia Chone Malembo amesema mgodi huo umeanza rasmi uzalishaji wa dhahabu mwezi Machi mwaka huu ambapo zaidi ya kilo 49 za dhahabu zimezalishwa na mgodi katika kipindi cha mwezi mmoja kufikia sasa na inatarajiwa kuuzwa kwenye masoko mbalimbali hivi karibuni.


"Kwetu sisi uwekezaji wa mgodi wa Shanta ni muhimu sana kwenye Mkoa kwa sababu ya kuongeza maduhuli kutokana na tozo mbalimbali ambazo watakuwa wakilipa kwa mauzo ya dhahabu katika malipo ya mrabaha na ada ya ukaguzi," amesema Mjiolojia Chone.

Pia, wananchi wa mkoa wa Singida watanufaika na mgodi wa Shanta kwa kuongeza kipato katika shughuli mbalimbali wanazozifanya kwenye maeneo ya mgodi na wale waliopata ajira kwenye mgodi.


"Mgodi wa Singida umekuwa na Sera nzuri sana ya utoaji wa ajira kwa wazawa na wakazi wa Kata ya Mang'onyi  na vijiji vyake vitano vinavyozunguka mgodi huo ambapo iliundwa kamati maalumu ambayo ilikuwa inaratibu zoezi la ajira," ameongeza Mjiolojia Chone.


Kwa upande mwingine, kutokana na ukubwa wa mgodi huo umeajiri watu wengi ambao hawakuweza kupata makazi kwenye mgodi huo na hivyo kuwanufaisha wakazi wa Mang'onyi wanaopata kipato kutokana na kupangisha nyumba kwa watumishi wa mgodi.


Hafla ya uwekaji jiwe la msingi ujenzi wa mgodi mpya wa kati wa Singida ilifanyika Oktoba 16, 2020. Mgodi wa Singida umekuwa mgodi wa pekee wa Kati kuanza uzalishaji mkoani Singida kwa kufanya uwekezaji mkubwa ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya mgodi, afya na miradi mbalimbali ya maendeleo ili watanzania wanufaike ra madini hayo.

Comments