BURUNGE WAPATA TIBA KUONDOA MIGOGORO YA WANYAMA WAKALI KWENYE MAKAZI YA BINADAMU.

 BURUNGE WMA wapata tiba kupunguza mgogoro wanyamapori na Binaadamu

Na Lucas Myovela - Babati Manyara.

 

Viongozi wa Hifadhi ya jamii ya wanyamapori ya Burunge ,pamoja na viongozi wa halmashauri ya Babati,wamejifunza Mbinu ya Kisasa ya kutumia waya wa umeme kuzuia wanyamapori wakali kama Tembo na Simba kuleta madhara kwa binaadamu.

Viongozi wa hao Burunge WMA wakiwepo Wajumbe wa kamati ya uongozi (AA)wajumbe wa Bodi na viongozi wa halmashauri ya Babati na idara ya wanyamapori Mkoa Manyara,wamefanya ziara ya mafunzo ya siku mbili Ikona WMA kwa ufadhili wa Taasisi ya Chemchem Association, ambayo imewekeza shughuli za uhifadhi na Utalii katika eneo hilo n kupata fursa kujifunza.


Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Babati Anna Mbogo ambaye aliongozana na viongozi hao kwa ajili ya kujifunza namna ya kudhibiti wanyamapori waharibifu amesema, “nimevutiwa na njia hii ya kisasa inayolinda mazingira”amesema na kuongeza,


“Niitakaa pamoja na wataalamu wilayani Babati kutathimini gharama za kuweka uzio huo wa umeme ili kulinda ushoroba katika Hifadhi ya Burunge WMA ambao ni sehemu muhimu ya Ikolojia ya eneo hilo na kuwanusuru wananchi na madhara yanayosababishwa na wanyamapori wakali”amesema.


Katibu wa Ikona WMA Yusuph Manyanda amesema, licha ya kutumia mbinu mbalimbali ikiwemo Pilipili,doria ,Elimu na Ulinzi shirikishi kutoka katika makundi ndani ya jamii ili kupambana na wanyama vamizi na kusababisha madhara kwa wananchi lakini matumizi ya fensi ya umeme imekuwa na faida zaidi.


“Uwepo wa uzio huo uliojengwa na Kampuni ya Grumeti Fund umekuwa na matokeo chanya kwa hifadhi na wakazi kwa kuwa umezuia muingiliano, hali iliyopelekea wakazi wa eneo hilo kuanza tena shughuli za kilimo walizokuwa wameziacha kwa muda mrefu kwa hofu ya kuharibiwa mazao yao”amesema.


Emmanuela Galu Mjumbe wa Burunge WMA amesema, “jukumu limebaki kwetu kutoa elimu kwa wafugaji na wakulima waweze kufahamu njia mbalimbali za kudhibiti wanyamapori waharibifu ikiwemo njia ya kuwazuia kisasa bila kutumia nguvu kubwa”amesema.


Felix Mwasenga Afisa Wanyamapori Mkoa wa Manyara amewashukuru Taasisi ya Chem chem iliyowekeza Burunge WMA kwa kuwezesha ziara hiyo ya mafunzo imewasaidia kupata ujuzi utakaosaidia jamii ya Manyara kupunguza migogoro baina yao na wanyamapori 


Meneja wa Chem chem association ,Clever Zulu amesema ziara hiyo imekuwa na mafanikio makubwa.


Amesema pamoja na kupata mbinu za kisasa kulinda shoroba wamejifunza pia kutumia uzio wa umeme kudhibiti migogoro ya wanyamapori na Binaadamu.


"Naamini viongozi wetu wa Burunge WMA,Viongozi wa halmashauri Babati na mkoa Manyara watakwenda kuona njia bora ya kumaliza kabisa tatizo la migogoro ya wanyama na wananchi lakini kutunza shoroba"amesema.


Mwenyekiti wa Burunge WMA,Erick Lilayoni alipongeza Chemchem kudhamini mafunzo hayo lakini pia Ikona WMA kuwapa elimu nzuri.


"Tumejifunza mengi tutakwenda kuyatekeleza Burunge WMA ilo wananchi waendelee kunufaika na uhifadhi na Utalii lakini pia kuongeza mapato na kutatua migogoro.





Mwisho

Comments