SAKATA LA WATOTO WACHANGA WALIYO FARIKI NA KUNG'OLEWA MACHO, KUKATWA ULIMI NA KUCHA LAZIDI KUCHUKUA SURA MPYA

BABA MZAZI AENDELEA KUGOMA KUZIKA WANAE HADI ATAKAPO KAMATWA ALIYE HUSIKA. 

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Balozi Dkt. Batilda Burian amesema baada ya mazungumzo ya muda mrefu hatimaye Isaka Rafael ambaye ni Baba wa Watoto Mapacha waliofariki katika Kituo cha Afya Kaliua na kuzua taharuki baada ya kung’olewa macho, na kukatwa ulimi, amekubali kushirikiana na Serikali na leo uchunguzi wa kitabibu umefanyika katika Hospitali ya Wilaya ya Urambo.


Akifanya mahojiano na CG FM ya Tabora, Dkt. Batilda amesema licha ya kufanikisha zoezi hilo muhimu la uchunguzi lakini Baba huyo ameendelea na msimamo wa kukataa kuchukua maiti kwenda kuzika akidai ni mpaka atakapokamatwa Mtuhumiwa wa tukio hilo.


Aidha RC Batilda ameiomba Familia ya Watoto hao kuwekeza imani kwa Serikali na kuisitiri miili ya vichanga hivyo wakati juhudi za kuwapata waliohusika zikiendelea.


“Namuomba sanasana na nashukuru Ndugu wa Baba wote wanaunga mkono Mtoto akazikwe naomba Kijana wetu Isaka akubali kauli ya Ndugu zake na sisi Viongozi wa Mkoa na Wilaya akubali twende tukawasitiri wale viumbe wa Mungu”


"Tunamuhakikishia suala hili tunalichukulia kwa uzito wa hali ya juu ni suala linaufedhehesha Mkoa wetu na linachafua sura ya Mkoa kwamba tunahusishwa sana na masuala ya ushirikina kwahiyo tutahakikisha wale wote waliokuwa mule ndani siku ya tukio kwenye wodi ya Wazazi, awe Mzazi au Msaidizi wa Wazazi na wale Wakunga ikiwemo Mama mzazi wa Watoto wote tutawahoji”

Comments