KUMEKUCHA ONYO KALI KWA MASHIRIKA YASIYO YA KISERIKALI YANAYO FANYA UDANGANYIFU WA MAPATO KUTOKA KWA WAHISANI

SERIKALI KUZICHUKULIA HATUA ASASI ZA KIRAIA ZINAZOFANYA UDANGANYIFU.

Na Lucas Myovela.

ARUMERU: Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhe. Emmanuela Kaganda ametoa onyo kwa Mashirika yasiyo ya Kiserikali yanayofanya udanganyifu kwa kutokuweka wazi taarifa za mapato na matumizi ya fedha toka kwa wahisani, kwani hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao .

Akizungumza katika kikao cha jukwaa la Mashirika yasiyo ya kiserikali katika Halmashauri ya Wilaya ya Meru, Mhe.Kaganda amesema Wilaya hiyo itafanya Msako kubaini Mashirika yanayofanya kazi kinyume na utaratibu na yasioleta tija kwa jamii hivyo kukwamisha azma ya Serikali ya kuwaletea wananchi maendeleo kwa wakati.


Mhe.Kaganda ameyataka mashirika yote yanayofanya udanganyifu ikiwa ni pamoja na ubadirifu wa fedha za miradi toka kwa wahisa kuacha mara moja ambapo ameiagiza Halmashauri kufanya ufuatiliaji kujua bajeti na shughuli shughuli zinazofanywa na mashirika hayo.


" shirika linapata mamilioni ya fedha toka kwa wahisani linatekeleza mradi wenye thamani ya asilimia 1% ya fedha" amehoji Mhe Kaganda

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru Mwl.Zainabu Makwinya amesema utambuzi wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali unaendelea.Pia ameshukuru mashirika ambayo yanayoshirikiana na Serikali katika swala zima la maendeleo.

Kwa niaba ya Mashirika yasiyo ya Kiserikali Vicent Uhega ambaye ni Mwenyeki wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali na Mkurugenzi wa Shirika Voice of Youth Tanzania amesema mashirika hayo yataendelea kushirikiana na serikali kwa uwazi na ukaribu ili kuwaletea wananchi maendeleo .


Jukwaa hilo la Mashirika yasiyo ya Kiserikali limefanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru na kujumuisha wawakilishi wa Mashirika mbalimbali yasiyo ya Kiserikali yaliyopo katika Halmashauri ya Meru .

Comments