WAATHIRIKA WA MAFURIKO HANANG KUJENGEWA NYUMBA 101 NA SERIKALI

ENEO LILILO ATHIRIKA KUFUTWA KUWA ENEO LA MAKAZI TENA.

Na Lucas Myovela.

Msemaji Mkuu wa Serikali amesema Serikali ya Tanzania imeanza utekelezaji wa ahadi ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwajengea Waathirika wa maafa ya maporomoko ya tope Wilayani Hanang Mkoani Manyara jumla ya nyumba 101.


Akiongea na Waandishi wa Habari Jijini Dar es salaam leo January 05,2024, Matinyi amesema kuwa nyumba hizo 101 ni kuwapa pole na kurejesha makazi ya familia 89 ambazo nyumba zao zilithibitishwa kupotea kutokana na maafa hayo na nyumba 12 ambazo zilisalia katika eneo hilo ambapo wataalamu wameshauri ziendolewe katika eneo hilo na kujengwa katika eneo jipya ambapo itafanya jumla ya ujenzi wa nyumba 101 ili eneo hilo lisitumike kwa aajili ya makazi tena.


“Nyumba hizi zinajumuisha nyumba 89 zilizothibitika kupotea baada ya maafa haya yaliyo tokea tarehe 3 Desemba, 2023, pamoja na nyumba 12 ambazo Wataalamu wa Serikali wameshauri zibomolewe na eneo lake lisitumike kwa ajili ya makazi ama shughuli zozote za kiuchumi na kijamii" Alisema Matinyi.


“Serikali imetenga ekari 100 kwa ajili ya ujenzi wa makazi mbadala ya kudumu katika shamba la Waret lililopo kwenye eneo la Jeshi la Magereza, kwenye kijiji cha Gidagamowd, kata ya Mogitu, wilayani Hanang. Eneo hilo lipo umbali wa km 4.5 kutoka barabara kuu ya Babati-Singida, na km 21.2 kutoka mji mdogo wa Katesh kuelekea Singida”. Aliongeza Matinyi.


“Kazi zilizokamilika hadi sasa ni upimaji wa viwanja na usajili wa ramani ya eneo la ujenzi. Kuna jumla ya viwanja 269 vilivyopimwa ambapo viwanja 226 ni makazi pekee, viwanja 26 ni makazi na biashara na viwanja 17 ni maeneo ya huduma za kijamii kama zahanati 1, eneo la kuzikia 1, kiwanja cha michezo 1, eneo la wazi 1, viwanja vya maeneo ya ibada 3, ofisi ya kitongoji 1, soko 1 na Shule ya Msingi 1”. Alisisitiza Matinyi.


Aidha Matinyi alisema kuwa katika zoezi hilo hatua nyingine inayofuata ni umilikishaji wa viwanja kwa Waathirika, ukamilishaji wa ubunifu wa ramani za nyumba, gharama na zijengwe na nani lakini mpango ni kufanya kazi kwa mtindo wa operesheni kwa muda wa miezi mitatu tu ili waathirika wapate makazi mapya na shughuli zingine za ujenzi wa taifa ziendelee.

Comments