NAIBU WAZIRI TAMISEMI AAGIZA SHULE MPYA ZA SEKONDARI KUFUNGWA MIFUMO YA KIDIGITALI YA KUFUNDISHIA, APIGA MARUFUKU MATUMIZI YA KUNI KWENYE SHULE ZENYE MIUNDOMBINU YA NISHATI

🔺️SHULE MPYA ZA SEKONDARI ZIFUNGWE MIFUMO YA KIDIJITALI YA KUFUNDISHIA e-leaning.

Na Lucas Myovela - Longido, Arusha.

Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI anayeshughulikia Elimu, Mhe. Ruben Kwagilwa, amemwagiza Katibu Mkuu wa TAMISEMI, kuhakikisha shule mpya za sekondari maalumu za mchepuo wa Sayansi kufungwa mifumo ya kufundishia ya kidigitali (e-learning) ili kurahisisha ufundishaji sambamba na kukabiliana na uhaba wa walimu wa masomo ya Sayansi nchini.

Naibu Waziri, Kwagilwa ametoa maagizo hayo leo Jamuari 17, 2026 wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukaguamazingira ya ufundishaji na kujionea hali ya miundombinu kwenye shule ya Sekondari ya Longido Samia Girls, iliyopo Wilayani Longido, Mkoa wa Arusha. 


Ambapo Shule hiyo ya Longido Samia Girls ni miongoni mwa shule mpya 26 zilizojengwa nchini kote kwa lengo la kuinua elimu kwa wasichana hasa katika masomo ya sayansi.


Naibu Waziri Kwagilwa, ameeleza kuwa matumizi sahihi ya programu za TEHAMA yataongeza ufanisi katika ufundishaji ili kukabiliana na upungufu wa walimu wa masomo ya Sayansi sambamba na kuwasaidia wanafunzi kuelewa kwa urahisi na kuongeza kasi ya uelewa pamoja ufaulu.

"Kupitia mifumo ya TEHAMA, Serikali itashirikiana na Chuo cha Serikali cha Hombolo na kuhakikisha miundombinu hiyo inafungwa kwenye shule zote ili wanafunzi waendelee kusoma kwa bidii hata pale walimu wanapokuwa wachache". Amesema Kagwila.


"Uwepo wa mifumo hii ya TEHAMA itasaidia wanafunzi kote nchini kusoma kwa pamoja na kwa wakati hata kama mwalimu yupo mbali lakini wanaweza kuuliza maswali na kujibiwa kitu ambacho kitafungua uelewa mpana kwa wanfunzi na taifa kufikia malengo yake katika sekta ya elimu nchini". Ameongeza Kagwila.


Aidha Naibu waziri Kagwila, ameelekeza shule hizo kutumia nishati safi huku akibainisha serikali tayari imekamilisha ufungaji wa miundombinu ya nishati safi katika shule hizo, Pia amepiga marufuku matumizi ya kuni katika shule zote zilizounganishiwa miundombinu ya nishati safi, na kuzitaka shule zotenchini kuachana na kuni na kutumia nishati safi ya kupikia.


"Ni marufuku kupikia kwa kuni katika shule zote zilizounganishwa na nishati safi, matumizi ya nishati safi ni ajenda ya taifa lazima sote tuungane na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha taifa letu ni safi katika nishati za kupikia na kutunza mazingira". Amesema Kwagilwa.


Pia aliwaagiza wakuu wa mikoa, wilaya na wakurugenzi kusimamia kikamilifu zoezi la uandikishaji na uripoti wa wanafunzi wa darasa la awali na la kwanza, huku akitaka hatua zichukuliwe kwa wanafunzi ambao hawajaripoti ili kubaini changamoto zao.

Mkuu wa shule ya Longido Samia Girls, Mwalimu Esther Kobelo, akisoma taarifa ya Shule hiyo mbele ya Naibu Waziri wa TAMISEMI, Ruben Kwagilwa.




















Comments