DKT. MAHERA ATOA VIFAA VYA KUIMARISHA MIUNDOMBINU YA ELIMU BUTIAMA VYENYE THAMANI YA MILIONI 66..

🔺️AHAIDI KUBORESHA MIUNDOMBINU YA ELIMU KWA WANAFUNZI ILI KUPATA ELIMU STAHIKI KATIKA MAZINGIRA RAFIKI.

Na Lucas Myovela.

Mbunge wa jimbo la Butiama Mhe. Dkt. Charles Mahera amekabidhi vifaa vitakavyosaidia kuboresha miundombinu ya elimu katika Jimbo la Butiama na kuhaidi ataendelea kushirikiana na Serikali pamoja na wizara kuhakikisha miundombinu ya elimu inakuwa bora kwa wanafunzi kwa maendeleo ya taifa kuelekea Dira ya Taifa 2050.

Dkt. Mahera ameeleza kuwa kupitia Fedha za mfuko wa jimbo atazisimamia na kuelekeza katika maendeleo ya jamii katika nyanja zote ili kuhakikisha wananchi wa Jimbo la Butiama wanaondokana na changamoto mbalimbali ambazo zinazo wakabili kwa kuboresha miundombinu katika sekta ya Elimu, Afya, maji, Barabara za ndani pamoja na masoko.


"Matumizi ya fedha za mfuko wa Jimbo katika kuchangia Elimu ili kukuza, kuimarisha na kuendeleza elimu, leo nimegawa vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 66 kwa shule za msingi na sekondari wilayani Butiama, ikiwa ni hatua ya kuboresha mazingira ya kufundishia kwa walimu na kujifunzia kwa wanafunzi wetu". Ameeleza Dkt. Mahera.


"Katika zoezi hilo, tumekabidhi bati, misumari, saruji na mbao kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya elimu katika jimbo letu. Aidha, tumetoa vitabu vya masomo ya Sanaa na Sayansi kwa Shule za Sekondari vyenye thamani ya shilingi 2,700,000/= ili kuongeza ubora wa ujifunzaji na kuinua ufaulu wa wanafunzi". Ameongeza Dkt Mahera.

Aidha ameeleza kuwa Fedha zilizowezesha utekelezaji wa hatua hizo zimetokana na Mfuko wa Jimbo, ambao unaendelea kuwa chachu ya maendeleo ya elimu na ustawi wa Wana Butiama.


“Tutaendelea kushirikiana na kuhakikisha watoto wetu wanapata elimu bora katika mazingira rafiki na yenye motisha”. Amesisitiza Dkt. Mahera.




#ButiamaKwanza #ElimuNiMaendeleo #KaziInaendelea

Comments